Thursday 22 August 2013

SHEIKH PONDA AFIKISHWA MAHAKAMANI MOROGORO







Katibu wa taasisi na Jumuiya za Kiislam Tanzania Sheikh Ponda Issa Ponda mkazi wa Dar es salaam jana asubuhi amefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi mfawidhi mkoa wa Morogoro kwa usafiri wa helkopta ya jeshi la polisi kujibu shitaka linalomkabili.
Ponda alifikishwa mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali wa jeshi la polisi wakiwa na mbwa baada ya kuwasili kwa helkopta hiyo iliyotua majira ya saa tatu subuhi katika uwanja wa Gofu mjini Morogoro ikitokea jijini Dar es salaam.
Wakili wa Serikali, Bernard Kongola alisoma mashitaka matatu dhidi ya Sheikh Ponda mbele ya hakimu mkazi Mfawidhi mkoa wa Morogoro Richard Kabate alisema, mnamo Agosti 10 mwaka huu katika eneo la Kiwanja cha Ndege  manispaa ya Morogoro Ponda  aliuambia umati wa watu uliokusanyika kwenye mkutano wa hadhaza “ndugu waislamu msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti kwani kamati hizo zimeundwa na Bakwata ambao ni vibaraka wa CCM na serikali na kama watajitokeza kwenu watu hao na watajitambulisha kwamba wao ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, fungeni milango na madirisha ya msikiti yenu na muwapige sana” 
 
Kongola aliimbia mahakama hiyo kuwa kauli hiyo iliumiza imani za watu wengine na kwamba hatua hiyo ni kinyume cha agizo la mahakama ya hakimu mkazi Kisutu  Dar-es-salaam iliyotolewa na hakimu V. Nongwa, Mei 9 mwaka huu ambayo ilimtaka Ponda ndani ya kipindi hicho cha mwaka mmoja kutohubiri mambo ya uchochezi ambayo ni kinyume na kifungu cha sheria namba 124 cha mwaka 2002, shitaka ambalo alikana.
Katika shitaka la Pili, Ponda alidaiwa, Agosti 10 mwaka huu katika eneo la Kiwanja cha Ndege manispaa ya Morogoro na mkoa wa Morogoro aliwaambia waislam serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi kwa 
kuwaua, kuwabaka, na kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni waislamu lakini serikali haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo walipokataa mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni wakristo na kusema maneno hayo  yaliumiza imani za watu wengine ambapo ni kinyume cha kifungu cha sheria 129 cha mwaka 2002 shitaka ambalo pia Ponda alikana.
 
Kwa upande wa utetezi, Ponda alikuwa akitetetewa na wakili Ignas Pungu na Bantalomeo Tarimo, huku upande wa serikali walikuwa wanaongozwa na Benedict Kongola, Gloria Rwakibalila, Asnab Mhando
 
Shekhe Ponda Issa Ponda aliwasilishwa kwa helkopta ya jeshi la polisi katika uwanja wa Gofu mjini morogoro akiwa chini ya ulinzi wa polisi na kupandishwa katika gari maalum ambalo liliongozana na magari mengine matatu ya polisi huku ulinzi ukiwa umeimalishwa katika eneo la mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Morogoro wakiwemo askari wa Kikosi cha Kutuliza ghasia, wa  upelelezi usalama wa taifa pamoja na mbwa wa jeshi la polisi wakati shughuli za kazi katika mahamaka hiyo na ofisi za jirani zikiwa zimesimama kwa muda.
 
Alifikishwa uwanja wa mahakama  majira ya saa 5.00 kamili asubuhi magari yalisimama kwa takribani  dakika 30 ndipo askari walishuka kwenye gari na kumfungulia mlango kisha kushuka na kuongozwa kwenye mahakama ya wazi ya hakimu mkazi mfawidhi  mkoa wa Morogoro huku umati wa wananchi ukiwa umefurika mahakamani hapo na kushuhudia kilichokuwa kinaendelea.
Baada ya Kusomwa kwa mashtaka yote matatu wakili wa serikali aliiambia mahakama kuwa upelelezi wa kesi umekamilika na kupanga kesi kuanza kusikilizwa septemba 2 mwaka huu ambapo kwa upande wa utetezi uliomba mahakama kupanga kuanza kusikilizwa kwa kesi agosti 26 mwaka huu hali ambayo ilimlazimu hakimu Kabate kuwapa muda wa kujadiliana ambapo walitumia dakika tano kujadiliana na kurejea mahakamani na kupanga kuanza kusikilizwa kesi agosti 28 mwaka huu.
Mawakili wa upande wa utetezi walisema sababu za kuomba terehe hiyo ya kusikilizwa kwa kesi kwa kile walichoeleza kuwa mteja wao bado ni mgonjwa na anahitaji kupatiwa matibabu ya mara kwa mara hivyo anahitaji uangalizi.
 
Hata hivyo mahakama ilipomalizika hali ya ulinzi iliendelea kuimarishwa na kupandishwa kwenye gari maalum alilopanda na kuelekea kwenye uwanja wa Gymkana majira ya saa sita mchana  na kupandishwa kwenye helkopta kwa ajili ya kurejeshwa gerezani jijini Dar-es-salaam. 

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako