Thursday 25 July 2013

JUMA KASEJA ATOA LA MOYONI


Aliyekuwa golikipa namba moja na nahodha wa Taifa Stars Juma Kaseja ametoa la moyoni akisema atakuwa tayari kutaja timu atakayoichezea msimu ujao baada ya kutoka Kampala nchini Uganda alikokwenda na timu ya taifa ya Tanzania
Kaseja amesema tayari anajua anachokifanya na atakuwa wazi atakapocheza msimu ujao baada ya kumaliza majukumu hayo ya timu ya taifa inayosaka tiketi ya kucheza fainali za mataifa bingwa barani Africa CHAN dhidi ya Uganda The Cranes, mchezo utakaochezwa Jumamosi wiki hii kwenye uwanja wa Nelson Mandela.
Golikipa huyo ambaye alikuwa chaguo la kwanza la makocha wote waliopita kwenye klabu ya Simba na pia ndiye aliyekuwa nahodha wa klabu hiyo kabla ya mkataba wake kumalizika na viongozi wa klabu hiyo wamesema hawatamuongeza mkataba.
Kaseja amesema kuna timu nyingi zimejitokeza kuitaka saini yake ikiwemo vilabu vya ndani na nje ya nchi lakini mara kadhaa imekuwa ngumu kukubaliana navyo kwasababu viko chini ya dau analolitaka.
Hata hivyo amesema pamoja na baadhi ya timu zilizojitokeza kuwa na dau dogo lakini kuna timu nyingine zimefika dau lakini bado hajamalizana na timu yoyote akiendelea kutafakari na atakaporejea kutoka Uganda atakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuweka wazi kila kitu.
Kaseja amedumu kwenye klabu ya Simba kwa zaidi ya miaka 10 akijiunga kutokea Moro United na alicheza kwa msimu mmoja katika timu ya Yanga.
Amesema ameifanyia mengi makubwa klabu ya Simba na anaamini maamuzi hayo yaliyofikiwa yanafungua milango mingine katika maisha yake huku akiwashukuru wale wote wanaomtakia mema na wale wanaompiga mizengwe, yote akimuachia Mungu. 
Ukiondoa Moro United,Kaseja amechukua ubingwa wa ligi kuu akiwa na Simba na akiwa na Yanga lakini ikumbukwe pia mwaka 2001 aliibeba Simba mpaka hatua ya makundi ligi ya mabingwa barani Africa mbele ya Zamalek ya Misri.

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako