Thursday 13 June 2013

WATU SITA WAUAWA KASKAZINI MWA KENYA

Watu sita, wakiwemo wanafunzi wa wawili wameuawa kwenye shambulio la kuvizia, Kaskazini mwa Kenya karibu na mpaka wa Somalia.
Ripoti zinasema kuwa watu waliokuwa wamejihami kwa bunduki walishambulia kwa risasi lori mooja iliyokuwa ikielekea wilaya ya Mandera.
Eneo hilo limekumbwa na vita vya kiukoo pamoja na mashambulio kutoka kwa wapiganaji wa Kiislamu wa Al-Shabaab, ambao wana uhusiano na kundi la kigaidi la al-Qaeda.
Mwaka wa 2011, Kenya ilituma maelfu ya wanajeshi wake nchini Somalia kupambana na wapiganaji hao wa Al Shabaab.
Hata hivyo wanajeshi hao wa Kenya sasa wamejuishwa kwenye kikosi cha kulinda amani cha Muungano wa Afrika AU, kilicho na zaidi ya wanajeshi elfu kumi na nane nchini Somalia.
Mvulana na msichana mmojo ambao ni wanafunzi katika shule moja ni miongoni mwa waliouawa katika shambulio hilo lililotokea siku ya Jumanne.
Afisa mkuu wa polisi katika eneo hilo Joseph Tenai amethibitisha tukio hilo na kusema kuwa uchunguzi umeanzishwa kufuatia tukio hilo.
Manusura wa shambulio hilo wanasema, washambuliaji hao waliwavizia kutoka msituni na kuanza kulishambulia gari hilo kwa risasi.
Watu wanne waliuawa papo hapo.
Eneo hilo linapakana na Somalia katika upande wa Mashariki na Ethiopia katika upande wa Kaskazini.
Eneo hilo ni kame na idadi kubwa ya watu ni wafugaji wa mifugo wa kuhama hama na hakuna ulinzi wa kutunzo kutokana na idadi ndogo ya maafisa wa polisi.
Zaidi ya wakimbizi laki tano waliokimbia mapigano nchini Somalia wamepewa hifadhi katika kambi kubwa zaidi ya wakimbizi ya Daadab iliyoko katika eneo hilo la Kaskazini.
Katika miezi ya hivi karibu zaidi ya watu 30, wameuawa kwenye mapigano ya kiukoo katika eneo hilo.
Wiki iliyopita watu wawili waliuawa na wasichana wawili kutekwa nyara na watu wasiojulikana, katika eneo hilo.

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako