Thursday 17 October 2013

HUU NDIO UTAJIRI WA DANNY DAVID MRWANDA


Mrwanda anasema: “Kama mchezaji, nimejifunza kutokana na mazingira kupitia maisha wanayoishi wachezaji wengine waliotutangulia, nikakuna kichwa, nikajipanga.”  
MAISHA yanahitaji kitu gani tena? Ukiwa na akili na ukiitumia vizuri akili yako, utapiga bao la maisha. Hiki ndicho alichokifanya straika Mtanzania, Danny David Mrwanda. Ndio maana marafiki zake huwa wanamtania kwa kusema kuna ‘Mrwanda mmoja tu duniani.’

Si kosa kusema, Mrwanda ni milionea, kutokana na utajiri alionao anaweza kuishi maisha yoyote anayotaka bila hata kucheza soka. Kazi yake ni soka, fedha anazopata kutokana na soka kama usajili, mshahara na posho aliwekeza na sasa ukimtaja Mrwanda unamzungumzia mwanasoka mwenye mali za maana.

Anaweza kuingiza zaidi ya Sh350,000 za Kitanzania kwa siku sawa na Sh15 milioni kwa mwezi, kupitia vitega uchumi vyake vya biashara anazomiliki Tanzania.
Mrwanda alishtuka mapema na kupanga mambo yake, alitunza pesa na kufanya mambo ya maendeleo akiogopa kuumbuka baada ya kustaafu soka kama inavyotokea kwa wachezaji wengi.
Mrwanda anasema: “Kama mchezaji, nimejifunza kutokana na mazingira kupitia maisha wanayoishi wachezaji wengine waliotutangulia, nikakuna kichwa, nikajipanga.”

Utajiri wake
Maisha anayoishi Mrwanda jijini Dar es Salaam anastahili kuitwa staa na profesheno wa ukweli. Anamiliki nyumba kubwa ya kisasa iliyopo Kisukuru, Tabata, Dar es Salaam. Kwa haraka makadirio ya thamani ya mjengo huo ni Sh 200 milioni.
Anamiliki usafiri wa nguvu aina ya Nissan Murano, gharama yake ni kama Sh60 milioni.  Mbali na hivyo, anavyo viwanja vinne vyote viko jijini Dar es Salaam kati ya hivyo viwili ameshaanza kujenga na shamba la ekari moja lililopo King’azi, Kinyerezi, Dar s Salaam.

“Mpango wangu ni kujenga nyumba za biashara kama hapa (anaonyesha kiwanja kimoja ambacho kipo karibu na nyumba anayoishi hapo Kisukuru), unaona nimeanza kujenga fremu za duka kwanza huku, kule kwingine naangalia kwanza, naweza kujenga nyumba ya kulala wageni au kupangisha.
“Lile shamba kule bado nalima mazao mbalimbali na kufuga tu, ila nina mpango mkubwa hapo baadaye kwa sasa naangalia kwanza upepo ili nifahamu niweke kitu gani kitakachoniingizia kipato,” anasema Mrwanda.
Mbali na ardhi, ukikutana na daladala yoyote kwa nyuma imeandikwa  ‘Mrwanda The Straika’ kwa chini ‘Maximo’ na mbele ‘Royal Prince’  usijiulize mara mbili kutaka kujua ni za nani? Ni mali ya Mrwanda.
Mrwanda ndiye mmiliki wa daladala hizo, anazo nne, mbili zinafanya safari za Mwenge-Kariakoo na nyingine Mwenge-Posta. Kila daladala moja, inapeleka hesabu ya Sh85,000 kwa siku, ukizidisha mara nne idadi ya daladala hizo ni Sh340,000 kwa siku.

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako