Friday 24 January 2014

MATANGENEZO YA DARAJA LA MKUNDI BEREGA DUMILA YAKIENDELEA



Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ametembelea eneo la Dumila ambako mvua kubwa zinazoendelea kunyesha zimesababisha mafuriko ambayo yameharibu sehemu ya barabara kwenye daraja la Mto Mkundi mkoani Morogoro.
Akiwa katika eneo hilo Waziri Magufuli baada ya kujionea hali halisi amemwagiza Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tanroads Mhandisi Crispianus Ako pamoja na Watendaji wengine waandamizi kutoka Tanroads na Wizara ya Ujenzi kuwepo hapo muda wote wakati kazi za kurejesha mawasiliano zikiendelea ili kuhakikisha kuwa matengenezo hayo yanakamilika mapema tayari kwa magari kuanza kupita.
 Katika hatua nyingine Mhe. Magufuli ametahadharisha kuwa magari yanayoruhusiwa kuzungukia barabara mbadala inayoanzia Dumila kupita Kilosa hadi Morogoro ni mabasi ya abiria na magari mengine yasiyozidi uzito wa tani 10. “Barabara hii mbadala ya kupitia Kilosa, Melela hadi Morogoro ni ya mkoa na iko katika kiwango cha changarawe ikiwa na madaraja yenye uwezo wa kubeba chini ya tani 10 tu, hivyo magari mengine yote yenye uzito zaidi ya hapo yatabidi kusubiri wakati tukiendelea na jitihada za kuifungua barabara hii mapema iwezekanavyo” amefafanua Mhe. Magufuli.
Daraja la Mkundi liko kiasi cha kilometa 65 kutokea Morogoro mjini kuelekea Dodoma na mikoa mingine ya kati hadi magharibi mwa nchi yetu ikiungana na nchi jirani za Uganda, Rwanda, Burundi na Jamhuri ya watu wa Kongo.

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako