Wednesday 18 December 2013

SANAMU KUBWA YA MANDELA YAZINDULIWA


Sanamu kubwa zaidi duniani ya Nelson Mandela imezinduliwa katika mji mkuu wa Afrika kusini Pretoria siku moja baada ya rais huyo wa zamani kuzikwa. Sanamu hiyo iliyotengenezwa kwa shaba ina urefu wa mita tisa na ina uzani wa tani nne unusu. Ilizinduliwa katika bustani la majengo ya bunge na inaonyesha Nelson Mandela akihimiza umoja na maridhiano. 
Sanamu hiyo yenye mikono ya Mandela ikiwa wazi ilinuia kuonyesha Mandela alivyoliunganisha taifa zima kwa mapenzi yake. Marehemu Mandela alipewa mazishi ya kitaifa nyumbani alikozaliwa katika kijiji cha Qunu Jumapili Familia ya Madiba, viongozi wa ANC, viongozi wa Afrika na maafisa wengine wakuu walihudhuria mazishi hayo katika kijiji cha Qunu mkoani Cape Mashariki. Kifo cha Mandela kilifuatwa na maombolezi ya siku kumi na sherehe za kukumbuka maisha ya Mandela aliyefariki akiwa na umri wa miaka 95. 
 
Bendera ya nchi hiyo ilirejeshwa kupepea katika urefu wake wa kawaida. Mandela anakumbukwa kwa juhudi zake za kupatanisha wananchi na kupigia debe msamaha miongoni mwa watu na ndio maana leo ikawa siku iliyotengwa kwa ajili ya uzinduzi wa sanamu hiyo. Wakati wa utawala wa wazungu, terehe 16 Desemba ilijulikana kama siku ya kuwakumbuka mashujaa wa Afrikaners walioshinda vita dhidi ya jeshi la Zulu mwaka 1883. Zaidi ya karne moja baadaye mwaka 1961, Mandela alizindua jeshi lake la Umkhonto we Sizwe kupigana dhidi ya utawala wa wazungu. 

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako