Friday 6 February 2015

UWANJA WA MALABO WAGEUKA VITA BAADA YA WENYEJI GUINEA KUPIGWA 3 BILA NA BLACK STARS



NDOTO za wenyeji Equatorial Guinea kunyakua Kombe la Mataifa ya Afrika zimeyeyuka usiku wa jana baada ya kufungwa mabao 3-0 na Ghana Uwanja wa Malabo.

Black Stars inayofundishwa na kocha wa zamani wa Chelsea, Avram Grant ilipata mabao yake kupitia kwa Jordan Ayew kwa penalti dakika ya 42, Mubarak Wakaso dakika ya 45+1 na Andre Ayew dakika ya 75.

Baada ya bao la tatu, huku Ghana wakiendelea kuwashambulia wenyeji, zikiwa zimesalia dakika nane mchezo kumalizika, mashabiki wa Guinea walianza kurusha chupa uwanjani na pia kuwapiga nazo mashabiki wa Ghana, ambao walilazimika kuvamia uwanjani kunusuru maisha yao.

Polisi walilazimika kutumia hadi helikopta kuwaondoa uwanjani mashabiki wa Guinea na baada ya nusu saa hali ilipotulia Uwanja ulikuwa kama mtupu na refa Eric Castane akamalizia mchezo.  

Ghana sasa itamenyana na Ivory Coast katika fainali ya AFCON 2015 Jumapili, wakati hatma ya wenyeji na mchezo wa mshindi wa tatu dhidi ya DRC haijajulikana, kwani kuna uwezekano wakapewa adhabu kali na CAF. 

No comments:

Post a Comment

Ahsante kwa Maoni yako